WABUNGE KENYA WADAIWA KUTUMIWA PICHA ZA UTUPU
- Fahari News
- Mar 15, 2018
- 1 min read

Wabunge katika Bunge la Kenya, wamezungumzia namna wanavyoandamwa na wahalifu wa mitandaoni, wanaowataka watoe fedha na kuwatumia picha za utupu.
Kiongozi wa waliowengi bungeni, Aden Duale na Mbunge wa Kiminini, Chris Wamalwa waliliambia Bunge jana namna mwanamke mmoja, ambaye hawakumtaja, anavyowafanya wahofie kutumia simu zao hadharani kwa kuwa imekuwa akiwatumia picha za utupu.
“Kuna mwanamke ambaye ana namba za simu za wabunge wote na hututumia picha za utupu mara kwa mara,” alisema Duale.
Naye Wamalwa alisema swala hilo ni muhimu kwa sababu limevunja familia nyingi na ni sharti likabiliwe. Mbunge huyo wa Kiminini alieleza namna siku moja alivyopokea picha za utupu akiwa ameketi na mbunge mwingine mwanamke bungeni na alipozifungua alihisi aibu kubwa.
Kiongozi wa wachache bungeni, Junet Mohamed alisema wabunge wanaume wamekuwa wakihangaishwa zaidi na wahalifu wa mitandaoni kulinganisha na wezao wa kike.
“Nimepokea picha za utupu katika simu yangu ambazo ni chafu kuangalia. Picha hizi ni hatari hali ya kuwa unaombea zisitumwe wakati mtoto anapochukua simu yako.
“Tatizo kubwa tunalokumbana nalo ni uhalifu wa mitandaoni tumehangaishwa kutongozwa huku kazi za wanasiasa wengine zikipotea kutokana na uhalifu wa mitandaoni,” alisema.
Mwakilishi wa wanawake katika Kaunti ya Baringo, Kaptuya Cheboiwo, alisema si wabunge wanaume pekee ambao wamekuwa wakiandamwa, bali pia wa kike.
“Wabunge wanaume wanadhani wanatongozwa kila mahala. “Ukiwa na mume ambaye hawezi kuhimili uzito wa tatizo hilo, huenda ukapewa taraka,” alisema Cheboiwo.
Wabunge hao wamemtaka Mkuu wa Jeshi la polisi, Joseph Boinnet, kufika mbele yao katika kipindi cha siku saba zijazo ili kuelezea njia anazotumia kukabiliana na tatizo hilo la mtandaoni.
Comments